Saturday, December 27, 2008

Najua tumefanya mengi katika mwaka huu unaoeleka kumalizika. Ni jukumu la kila mmoja kutengeneza mipango kwa ajili ya 2009

Ninajiandaa kuiboresha zaidi blog hii

HERI YA KRISMAS NA MWAKA MPYA


Kwa wasomaji wote wa blog hii, maneno haya hapa chini ni kwa ajili yenu wote


May The Almighty God reward you greatly in your future endevours and give your heart's desires.


All unfulfilled ends in 2008 should emerge and get you shine in the coming year

Thursday, October 09, 2008

USISHANGAE! HATA HILI LINAWEZA KUWA KWELI

Nimeipata toka kwa mdau mmoja na nimeona na wewe nikufahamishe.


Familia moja ilishangazwa pale walipopokea jeneza la marehemu mama yao aliyefariki nchini Marekani. Lilitumwa na mmoja ya watoto wake wa kike. Mwili ndani ya jeneza ulikuwa umesongwa sana ndani ya jeneza kiasi kwamba uso wa marehemu ulikuwa umegusa kioo cha jeneza! Walipofungua jeneza, walikuta barua juu ya merehemu, iliyosomeka namna hii: 'Wapendwa ndugu zangu, nimeutuma mwili wa mama yetu kwa ajili ya mazishi, kwani imekuwa siku zote hamu yake kubwa kuzikwa nyumbani Ileje, katika nyumba ya ukoo. Samahani sikuweza kuja na mwili kwani nimenyimwa likizo kwani kuna upungufu wa wafanyakazi hapa kazini mwezi huu. Ndani ya jeneza, chini ya mwili wa mama, kuna makopo 12 ya samaki wa makopo, paketi 10 za supu ya Royco na chupa 8 za jam ya maembe.Mgawane hivi kwa jinsi mtakavyoamua nyinyi. Katika miguu ya mama kuna pea moja ya viatu vya Reebok namba 9 kwa ajili ya mtoto mkubwa wa Mwakajinga. Pia, kuna pea mbili za viatu kwa ajili ya watoto wa Mwakipesile na Ipiana , natumaini nitakuwa sijakosea namba za miguu. Nimemvalisha pia mama American T-shirts 6, kubwa kabisa ni kwa ajili ya Mwakibibi, na zinazobaki ni za watoto wake. Hizo jeans mpya 2 ambazo mama amezivaa ni za wavulana Mwakatumbula na Mwakitobe. Hiyo Swiss watch mkono wake wa kushoto ni zawadi ya Rhoida kwa ajili ya sikukuu yake ya kutimiza miaka 21. Anti Queen, hizo heleni, mkufu na pete ambazo mama amevaa ni zako. Hizo soksi 6 ambazo mama amevaa wagaiwe wajomba. Tafadhali mgawane kama nilivyosema na kama kuna kitu kingine mnahitaji, basi mnieleze kwani hali ya baba nayo siku hizi si nzuri sana .Dada yenu mpenzi, Mama Mpoki

Monday, June 23, 2008

MAXIMO ANA MCHANGO MDOGO SANA KATIKA SOKA LA TANZANIA

Najua wapo wanaoamini kuwa ufanisi wa Taifa Starz umechangiwa na kocha wa kibrazil aliyeletwa na JK. Kwangu mimi hali ni tofauti na wote wanaotangaza kuwa Tanzania imetangazwa na Maximo.

Kuna vitu kama viwili ambavyo ndivyo vimeifanya Taifa stars ifikie kiwango hiki ambacho hata hivyo hakijafikia kiwango kilichooneshwa na timu yetu ya taifa kwenye miaka ya 80. Vitu hivi ni kama vifuatavyo:-

Sapoti kubwa ya serikali kwa timu: Hii ndiyo chachu kubwa sana ya timu yetu kufanya vizuri. Wakati mbrazil anakuja si kweli kuwa timu yetu ilikuwa mbovu kiasi cha kusema kwamba alitukuta tuko wodi ya wagonjwa mahututi. serikali miaka ile baada 80 haikuonesha kipaumbele katika kusaidia timu ya taifa. Rais JK alipoingia madarakani kuliendana na mabadiliko makubwa katika utendaji wa TFF (zamani FAT) na hivyo alitambua kiu wa watanzania kuwa ni maendeleo ya soka na hapo ndipo alipoanza kuisadia timu kwa kuipatia kocha na misaada mingine.

Mfumo wa soka letu ulitengemaa na shurani kubwa ziende kwa shule mbalimbali nchini ambazo zilikuwa stari wa mbele kuwapa nafasi vijana wenye vipaji vya soka kujiunga na shule hizo na kuendeleza vipaji vyao, mfano wa shule hizo ni Makongo na Jitegemee kwa DSM. Mikoani napo vijana wenye vipaji walikuwa wanaangaliwa kwa ukaribu zaidi.

Kutokana na muundo mzima wa uongozi wa chama cha soka Tz wadau mbalimbali walijitokeza kuisadia timu ya taifa kwa hali na mali kama tunavyoshuhudia wafadhili mbalimbali ambao wamekuwa wakitoa pesa zao na kudhamini timu ya taifa. Kwa kuwataja kwa uchache hawa ni TBL, Serengeti, NMB na NBC pamoja na makampuni na watu binafsi.

Ukiangalia sababu hizi utagundua kabisa hata walimu wetu wa bongo wangekuwa wakipewa sapoti kama hii wasingeshindwa kuifikisha timu hii hapa ilipo.

Unaweza kufikiria hili na kutoa maoni yako
USISEME UNA MATATIZO

Wadau hii nimeitoa kwa Mzee wa Sumo.

Mzee Kidevu kanitumia hii!Jamaa wawili walikutana kwenye kituo cha basi wakafanya mazungumzo.

Mmoja aling'ang'nia kuzungumzia kero za familia yake hatimaye mwenzake akasema " Unadhani familia yako ina matatizo?"Basi sikiliza kisa hiki.

"Miaka michache iliyopita nilikutana na mwanamke mjane aliyekua na binti mkubwa tu na tukaamua kuoana. Baadaye baba yangu akamuoa binti yangu wa kambo hivyo huyo binti yangu wa kambo akawa mama yangu wa kambo na Baba yangu akawa mtoto wangu wa kambo wa kiume ambapo mke wangu akawa mama mkwe wa mkwe wake.Baadaye binti yamke wangu yaani binti yangu wa kambo alipata mtoto wa kiume. mtoto huyo wa kiume alikua ndugu yangu kwa sababu tulichangia baba mmoja. lakini kwa vile alikua ni mtoto wabinti wa mke wangu papo hapo akawa mjukuu wa mke wangu na mimi nikawa babu yake ndogo wangu.

Lakini hayo yote yalikua si kitu mpaka mimi na mke wangu tulipopata mtoto wa kiume. Sasa msichana ambaye ni ndugu wa mtoto wangu huyo wa kiume kwa kuchangia mama yao mmoja, akawa pia bibi yake. Hali hiyo ilimfanya pia baba yangu kua shemeji wa mtoto wangu ambaye ndugu yake wa kike kwa upande wa mama yao ndie mke wake baba yangu. Kwa hiyo mimi ni shemeji yake mama yangu wa kambo ambapo mke wangu ni mama mdogo (anti) wabinti yake mwenyewe . Mtoto wangu wa kiume ni mpwa wa baba yangu ambapo mimi nikawa babu yangu mwenyewe.

SWALI.Je, unadhani mpaka hapo wewe una matatizo ya kifamilia? Acha kulalamika
HIVI IKIWA NDIVYO, ITAKUWAJE!!!

Hii nimeipata toka kwa rafiki yangu aliyeko Nairobi na ninapenda kuiweka hapa kama ilivyoletwa

Kuna mdau eti laleta hii, jamani kutania viongozi...
Nafurahi kuwajulisheni nyote kwamba kuna vyuo kumi vimefunguliwa maeneo mbalimbali nchini, vikitoa kozi mbalimbali na kubeba majina ya watu maarufu kama ifuatavyo:

* Benjamin Mkapa Institute of Political Entrepreneurship and Openness

* David Balali School of Central Banking and Foreign Debt Management

* Andrew Chenge College of Applied Contractual Law

* Ali Hassan Mwinyi University of Inflation Control

* Karamagi Institute of Mining Licensing and Administration of Mining Contracts

* Zakia Meghji college of Tourism and Protection of Public Funds and Natural Resources

* Ditopile Mzuzuri School of Conveyance and Welfare of Public Drivers

* Mwalimu Nyerere University College of Privatization

* Mkono Intitute of Legal Fraud Prevention

* Lowassa School of Prevention of Fake Companies

Mimi nimefurahishwa na utani huu, sijui wewe

Thursday, April 17, 2008

UNAFIKI WA VIONGOZI WA DINI

Siongelei dhehebu moja ama mawili, naongelea viongozi wa dini zote za kigeni( ambazo hazina asili yake Afrika).

Makanisa yetu na misikiti yetu imekuwa ikipokea misaada mbalimbali toka kwa wafadhili wa ndani na nje. Misaada hii imekuwa ni kwa ajili ya maendeleo ya waumini wote.

Cha ajabu sasa ambacho msomaji unaweza kukubaliana nami ni kuwa, misaada hii imekuwa ikiishia matumboni mwa viongozi hawa ambao unapokutana nao njiani na maneno yao huku wakiosha mikono kila wanapoongea ni tofauti kabisa na matendo yao ya KIFISADI.

Tunapoongelea kuhusu ufisadi kwa viongozi wa serikali basi tusisahau kile kinachofanywa na viongozi wetu wanaovaa majoho na kanzu nzuri
UTAJIRI WA CHENGE

Kama kuna jambo ambalo linaongelewa sana kwa sasa hapa kwetu Tanzania ni suala zima la utajiri wa Chenge ambaye aliwahi kuwa mwanasheria mkuu wa serikali kwa kipindi cha miaka 10 katika zama za Mkapa.

Ni katika kipindi hiki ndipo taifa lilishuhudia uingiwaji mkubwa wa mikataba ambayo leo ndio inawasumbua watanzania.

Mikataba hii haikufungwa na kina chifu Mangungo bali ilifungwa na wasomi mahiri kabisa na wengine waliosoma vizuri katika vyuo vikubwa kabisa duniani na tena wakilipiwa na wanachi masikini kwa lengo moja tu kubwa, kuwatetea wananchi katika mambo mbalimbali ya kitaifa na kimataifa.

Lakini sasa tunachoshuhudia ni kinyume cha yale tuliyoamini, wale tuliowasomesha wamekuwa ni vinara wakubwa wa ufisadi na wamejaa viburi kiasi kwamba mtu anasema hawezi kuachia ngazi/madaraka kwa kelele za wananchi, swali langu hapa ni hili,

Hivi Mtanzania ni nani katika Tanzania!

Friday, January 25, 2008

HE! UNAFIKIRI HII NDIO NJIA SAHIHI?

Wakati wananchi wa sehemu fulani hapa Tanzania waliposikia kuwa 'gavana' ametolewa katika nafasi yake, baadhi ya wanajamii walivamia mashamba yake kilometa chache nje ya mji mkuu wa kibiashara.

Mimi kitendo hiki ninakiona ni cha kipekee kabisa, yaani mtu anapigiwa simu kuwa waende wakagawane mashamba ya fulani kwa kuwa tu huyo fulani ni fisadi! Wapi tunakwenda.

Sina hakika kama yale mwimbaji maarufu na mwanaharakati wa Marekani Tracy Chapman aliyoimba katika REVOLUTION 'mapinduzi ya watu wa chini' yanatimia.

Je!, wasiosema wameanza kusema! au wasiosikia wameanza kusikia, na nini kitafuata endapo mikononi watashika kilichokaribu yao!

Tusubiri
SAKATA LA BOT: WALIO KIMYA NAO WAMEKULA


Sidhani kama kuna yeyote mwenye uchungu na Tanzania anahitaji kuelezwa mwanzo wa mabilioni 133 yaliyotafunwa, kwa taarifa, pale kwenye benki kuu ya Tanzania. Kwa sasa kila mtu anamnyooshea mkono Ballali, gavana ambaye rais Kiwete ametengua uteuzi wake kama gavana.

Kwa maoni yangu, mimi nadhani mtu kama Ballali hawezi kuzitumbua pesa hizo peke yake hata kama angekuwa anakula kama funza. Kawaida ya funza huwa anakula na k****a wakati huo huo na ndio maana funza ni waharibifu wakubwa na mazao ya nafaka.

Hizi pesa zimeliwa na wengi, wengi tena sana ila kwa kuwa Ballali alimuonesha 'mungu' tumbo pale alipokanusha taarifa ya dk Slaa basi ndo leo umma umeamua kumuhukumu, na hakika hata kama atasafishwa vipi bado sisi tunamuona kama fisadi anayestahili kuhukumiwa na kufilisiwa kabisa na kama ndo ingekuwa katika zile nchi za kisoshalisti za kweli basi angeuawa hadjharani baada ya kuwa amewataja mafisadi wenzake.

Namtetea Ballali kuwa hizo pesa hajazila peke yake, amekula na wengi ambao wapo bado madarakani tena wanashikilia nyadhifa kubwa sana zinazowawezesha kusaini mikataba kwa niaba yetu huku wakitanguliza maslahi yao kwani hii ni kawaida yao. Tunaimba pamoja kijamaa wao wanacheza kifisadi.

Wengi waliokula wamekaa kimya huku wakijifanya hawahusiki na tena wengine bado ni 'wajumbe' wa bodi. Tunawasubiri hawa waseme kwa hiari la sivyo umma utawataka waseme wakiwa uchi
AFCON: TUNA MENGI YA KUJIFUNZA WATANZANIA


Tangu mwanzo wa mwaka huu 2008 si kwamba kila mtanzania amekuwa makini kufuatilia mashindani ya Mataifa ya Afrika yanayoendelea katika miji mbalimbali ya Ghana bali kila mtu na mpenzi wa soka duniani amekuwa makini kuna nini kinaendelea huko ambako miamba ya soka la kiafrika inakutana tangu kipite kindi cha miaka miwili ambapo Misri ilitwaa kombe hilo mbele ya 'Tembo' Ivory Coast.

Sitakuwa mchambuzi wa kuelezea mechi ambazo ndo kwanza zinaelekea katika hatua ya robo fainali bali mimi nitajaribu kujikita katika uga ambapo sisi kama watanzania tunaweza kuchota chochote kutoka Ghana.

Hakuna mtanzania ambaye anaweza kusahau namna timu yetu ya taifa ilivyoandaliwa kwa kupewa kila aina ya msaada na seriali ilivyoshindwa kushinda mechi muhimu za nyumbani na hivyo kutukosesha nafasi ya kuwakilisha nchi za jumuia ya Afika mashariki katika AFCON Ghana2008

Kikubwa ambacho ninaweza kuelezea mwanzoni kabisa ni namna ya kuthamini vipaji vya vijana wadogo bila kusahau uzoefu wa wachezaji wenye umri mkubwa lakini unaowawezesha kucheza soka. Pia nafasi ya wataalamu wa soka wazalendo katika kufanikisha mipango ya ushindi na si kushirikia na kutolewa katika hatua za mwanzo.

Tangu awasili kocha aliyetafutwa na serikali toka Brazil wengi tulikuwa na mawazo makubwa ambapo kila mtu alitazamia kabisa kuiona taifa stars ikicheza na kupata nafasi ya kwenda Ghana. Matarajio haya yalionekana kuwa kweli kutokana na namna serikali na wadau wengine walivyojitolea kuisadia timu hii ambayo mwanznoni ilionekana kama imetelekezwa.

Tatizo limejitokeza pale mtaalamu wa kibrazil alipoonesha kuwadharau watanzania akijifanya kuwa wakati alipokuja sisi hatukuwa tukijua mpira wowote na hivyo hatuwezi kumshauri katika kitu kinachoitwa soka. Kung'ang'ania kwake wachezaji chipukizi si vibaya lakini siku zote 'kijiji hakikosi wazee' lakini kuwatupa wazoefu ni tatizo kubwa. Katika safari mara zote ni lazima wawepo wanaoijua njia.

Vijana walioandaliwa vizuri tangu shuleni wana nafasi kubwa sana ya kuwa hodari katika fani nyingi, ni vizuri sasa kwa serikali na chama cha soka kuweka mikakati ili hata hiyo nafasi ya 2010 tuweze kuipata.

Ushauri wa wachezaji wazoefu, makocha wazalendo usidharauliwe. Hawa ni muhimu sana katika maendeleo ya soka letu. Tunashuhudia leo huko Ghana ambako timu nyingi zina nyota vijana wanaoungwanishwa na wakongwe.

Kwa kuwa mashindano bado yanaendelea na nzuri zaidi kwetu kuwa TVT inarusha matangazo 'live' tuna nafasi ya kujifunza mengi