Thursday, December 28, 2006

UNAFIKI WA WAANDISHI KTK KUPONGEZA MWAKA MMOJA WA KIKWETE MADARAKANI


Naaam, rais wa jamhuri ya muungano wa Tanzania JMK ametimiza mwaka mmoja tangu watanzania wamuamini katika kuwaongoza.
Mwaka mmoja si kipindi kizuri cha kuamua na kutoa tathmini ya kilichofanya na mtu tunayetegemea atuongoze kwa miaka mitano.
Waandishi wengi sana wamejitokeza kutoa na kuelezea mafaniko ya rais ndani ya mwaka huu mmoja, kila mmoja amemsifu na hii ni haki yake.
Tunajua kabisa rais amekuwa ni kipenzi cha waandishi wengi tangu enzi za mchakato wa uchaguzi na mpaka anakuwa rais, kwa hali hii si rahisi kwa watu waliokuwa wakimtukuza kama mtu mwajibikaji kuanza kumtenga na kueleza uhalisia.

Kwa upande wangu mimi sioni mafanikio yoyote kama baadhi ya waandishi wanavyotaka kutuaminisha na vyombo vyao, tazama hali ya usafiri kwa wakazi wa Kigamboni jirani kabisa na ikulu, siwezi kuyaona mafanikio ya kodi tunazoambiwa zinakusanywa kwa mabilioni wakati hakuna pantoni la uhakika, au hawa waandishi wanataka tufe baharini na waandike habari za kiongozi kuja kuwatembela ndugu zetu.

Hizi sifa anazopea JMK ziangaliwe tena kwani hakuna mabadiliko yoyote
HERI YA MWAKA MPYA

Wapendwa wasomaji wa blog hii, ninapenda kuwatakia baraka na mafanikio katika mwaka mpya wa 2007

Machweo inaahidi kutochoka kuwapa kile ambacho kinafaa kwa macho na akili zako, na kwa mwaka huu 07 tegemea makubwa zaidi

Saturday, December 23, 2006

HE!!! INAWEZEKANA.......

Juzi tumekuwa na kikao na mshauri wa wanafunzi (mwaka wa pili) kikao kilikuwa na mabo mengi yaliyoongelewa kikubwa ikiwa ni masuala mbalimbali ambayo wanachuo tunaona hayaeleki kwa kuwa hayajawekwa wazi na uongozi, kwa mfano suala la ada pamoja na utafiti , inakuwaje tunatoa pesa nyingi kila mwaka wakati utafiti tunaufanya kwa mwaka mmoja tu, pia tunalipa kodi kubwa ya pango (21000/=)kila mwezi ilhali huduma katika hosteli ni mbovu hususani ubovu wa makabati na upungufu wa matundu ya vyoo, hebuchukulia mfanowa hosteli ya Kizota juu ambayo inawakaazi karibu 70 lakini wote hawa wanategemea matundu mawili ya vyoo pamoja na milango minne ya mabafu!
Huduma ya chakula inatolewa na mtu mmoja tu, kwanini, ina maana hakuna watu wengine wa kutoa huduma kwa wanafunzi hasa ukizingatia kuwa mtoa huduma huyu hatoi huduma zinazoendana na namba ya wanachuo! Nani katika menejimenti anamlinda,kwanini serikaliya wanafunzi inasema kuhusu tatizo hili na blahblah toka kwa utawala ndo zinatawala!

Usiogope! haya yalijibiwa na mshauri ambaye kwa kweli alijitahidi sana kupunguza jazba za washikadau!
Hii ndo hali halisi iliyopo hapa chuoni na labda tutegemee mabadiliko kwani ukarabati uliochukua muda mrefu kuliko ujenzi ndo kwanza upo katika hatua za mwisho huku sisi wanachuo tukikosa maktaba na hivyo kufanya masomo yetu kuwa magumu hasa ukizingatia kuwa kutegemea maktaba za nje ni ghali kwa mabo ya kivuko ambacho kinachukua muda mrefu kuvusha watu huku ratiba ikiwa inatukaba kwa sana. Hii yote tisa ni hili lililotokea mkutanoni lilianza hivi...

baada ya dean kutoa nafasi kwa wanachuo kuuliza maswali na kutoa yote yanayowakereketa, akasimama mwanadada wa kozi ya Gender anaitwa dada Agnes, huyu ni mlemavu wa macho, haoni na kwa hapa chuoni yupo peke yake.

Aliposimama kuongea kila mtu ukumbini alinyamaza ili kusikiliza nini anasema, akiongea kwa sauti inayosikika masikioni kwa uzuri kabisa aliyatoa yake mengi na hasa lile ambalo yeye analiona kwamba kuwepo kwake hapa chuoni kumekuwa ni mzigo na inawezekana kwa kuwa chuo kimemuona ni mzigo kimeshindwa kuwapa nafasi walemavu kama yeye walioomba nafasi za masomo chuoni.

Yeye anakabiliwa na matatizo mengi katika kujisomea kwani gharama zote zinamwangukia yeye na chuo kinashindwa kumsaidia japo kwa kumtafutia karatasi za kuandikia. Alijaribu kuwapatia management anuani za mashirika ambayo yanawasaidia watu wenye matatizo kama yake lakini anashangaa hakuna chochote kilichoendelea, hajapata msaada.

Wote tulinyamaza na sikia jibu hili toka kwa Dean "si kweli kwamba chuo kinakuona wewe kama mzigo, kinajivunia kuwa nawe hapa na hata huwa naona wageni wanapotutembelea hapa huelezwa kuwepo kwako hapa". Naam, tulishukuru kwamba mshauri mwenyewe aliahidi kumsaidia dada huyu ili aweze kufanikisha kile kilichomleta hapa na kumwelewesha kwamba chuo hakina noma na kuwepo kwake hasa ukizingatia vyuo vyenyewe ndo hivi tu.

Kikao hakijaisha, nitakuwa nikikutaarifu kadri siku zinavyokuja kwani kuna fukuto ambalo linahitaji majibu na kwa hulka ya 'wakubwa' labda wanasubiri kitendo kitokee ndipo waseme wanavyoona ni sahihi kwa wanachuo kufanya

Miaka 45 ya uhuru: viongozi huru wenye suti za kikoloni

Naam, sherehe za kuadhimisha miaka 45 ya uhuru wa Tanzania (ipi ilipata uhuru, Tanganyika au Tanzania!) zimemalizika na kamati imevunjwa huku waziri mkuu akijipanga tena kuongea na wafanyabiashara ili wasaidie katika maandalizi ya sherehe zijazo.

Sherehe hizi zimefanyika kama kumbukumbu kuadhimisha uhuru wan chi yetu toka kwa wakoloni, waingereza ambao walipewa jukumu la kuwa waangalizi (Tanganyika became the british protectorate) wan chi yetu kwani Un haikuwa watawala na mnamo tarehe 9desemba 1961 bendera ya malkia ikashushwa na bendera yenye rangi nne kumaanisha Tanzania ikapandishwa.

Miaka 45 si mingi sanakwa miaka uhai wa taifa japo si haba kujivunia miaka hii tukiwa huru, na kwa kufikisha miaka hii hakuna haja ya kuacha kusheherekea kwa mbwembwe na majivuno mengi kuonesha ni nini maana ya kuwa huru.

Kusheherekea uhuru ni jambo muhimu sana yaani ni kama mtu wa kawaida anaadhimisha ‘birtday’ yake. Uhuru unamaanisha hali na uwezo wa kujiamulia mabo yako bila kuingiliwa na nchi au taifa jingine (sovereignity).

Sherehe za mwaka huu zimekuwa tofauti kidogo na zile zilizokuwa zikifanywa na wamu zilizopita. Hizi zilikuwa ni za ari mpya, nguvu mpya na ari mpya.

Zimekuwa ni tofauti kwa maana ya kwamba hizi zimeendana na mkesha wa nguvu uliooneshwa moja kwa moja na luninga ya taifa (TVT). Hii iliwapa nafasi watanzania wote kushuhudia sherhe hizi zilizoambatana na tatizo la kukatika katika kwa umeme..

Suala la kukatika kwa umeme siyo ishu iliyonishawishi na kunivuta kuandika kuhusu maadhimisho haya. Na wala sitaongelea suala la waziri mkuu kuwaomba wafanyabiashara wakubwa wajitokeze kuchangia na kufanikisha sherehe hizi zinazokadiliwa kugharimu bilioni moja na ushee pesa za kitanzania.

Wengi wameongelea kuhusu sherhe hizi, wapo waliohoji kuhusu suala la ni nchi gani iliyopata uhuru, mwandishi nizar visram yeye anashangazwa na tukio la waziri mkuu kukutana na wafanyabiashara ili wafanikishe sherehe hizi, kwake hili ni kama kuibinafsisha siku muhimu kwa watanzania wote.

Wanasosolojia nao hawakuwa kimya katika kuadhimisha shehere hizi zilizoshuhudia kwa mara ya kwanza madege yetu ya kivita yakipita kwa mbwembwe kusherehekea siku hii muhimu, wao wamehoji kuhusu ni nani hasa anayesheherekea siku hii kwa watanzania. Kwao matabaka yanayojitokeza nchini yanawafanya wahoji je ni kweli sherehe hizi ni za wote au ni kwa baadhi ya watanzania? Haya yameongelewa na si vibaya kuyajadili katika nchi hii inayoadhimisha miaka 45 ya uhuruhuju pengo kati ya maskini likiwa linaonekana wazi, maendeleo ya mijini na vijijini yakiwa na tofauti kubwa na huku mipango ya maendeleo vijijini ikijadiliwa na watu wa mjini.

Sasa turudi kwenye mada kwani isije nikaonekana nataka tu kujaza kurasa, lakini hata hayo niliyoyagusa ni muhimu yakajadiliwa na pia yatatuongoza katika kutambua mada ya leo.

Mavazi ni kitambulisho kikubwa cha uataifa wa mtu kama zilivyo pesa, wimbo wa taifa pamoja na ramani ya nchi. Leo hii ukiangalia nchi huru nyingine za kiafrika utaweza kuwatambua raia wan chi hizi kwa kuyaangalia mavazi wanayovaa, hebu chukua mfano wan chi za Nigeria, Ghana na afrika kusini. Tanzania na uhuru wetu bado hatuna vazi letu la taifa.
Katika mkesha wa kukaribisha saa sita,pale mnazi mmoja, wote tutakuwa mashahidi kwa namna viongozi wetu walivyokuwa wamependeza katika mavazi mazuri ya gharama toka magharibi. Kwa kifupi mavazi hasa yaliyokuwa yamevaliwa na viongozi yalikuwa ni kama tunaadhimisha uhuru wa nchi moja ya kimagharibi.


Tumeshuhudia umati wa watanzania waliohudhuria mkesha huu wakiwa na mavazi ya aina tofauti, huku wengi wasio jukwaani wakiwa ndani ya mavazi yaliyo kwenye ‘chati’ kwa sasa miongoni mwa watu wa chini ‘mitumba’.

Huku mkesha ukiambatana na ulipuaji wa baruti, tumeshuhudia viongozi wetu waliokuwa wakishuka toka katika magari makubwa nay a gharama wakiwa ndani ya suti nzito na za gharama. Tumeshudia viongozi wanaume wakiwa ndani ya suti nzito toka kwa wabunifu wa kimagharibi, mavazi ambayo yanaonesha kabisa kwamba inawezekana tukawa tunajitawala kwa kufikiri na kuvaa kimagharibi! Angalau mavazi yaliyokuwa yamevaliwa na wanawake viongozi yalijaribu kuonesha utamaduni wa kiafrika kwa kuuvaa Unaijeria na Ughana.

Kwa maisha ya leo yawezekana kabisa baadhi ya watu wakaona suala la mavazi ni ishu ndogo sana kiasi cha kujadiliwa katika kuadhimisha miaka 45 ya uhuru wan chi yetu. Kwangu hili ni suala la kujadili kwani kujitawala ni pamoja na kuonesha waliotutawala kwamba sasa sisi tuko huru yaani tunaweza hata kuwa na maamuzi katika mavazi ya kuvaa.

Uhuru una maana nyingi sana ikiwa ni pamoja na kuonesha hali ya kuwa na maamuzi katika utamaduni wako unaoongoza maisha yako ya kila siku. Mavazi ni sehemu ya utamaduni.
Utamaduni ni zaidi ya ngoma tunazozishudia zikialikwa kutumbuiza katika sherehe hizi. Ngoma kwa sasa kwa baadhi ya watu zimekuwa zikionesha ukale, kinachotamba sasa ni utamaduni wa ‘bongo fleva’. Tumeshuhudia kila mara vikundi vya ngoma vilipokuwa jukwaani havikupata mapokezi mazuri toka kwa hadhira lakini pale walipopanda ‘wanaume tmk’ wakiwa wamevaa mavazi ya kisasa kelele za kushangilia zililipuka. Huu ndio utamaduni tunaoushabikia sasa na miaka 45 ya uhuru.


Mwandishi mahiri katika suala la utamaduni wa mwafrika, mwanazuoni Kihumbi Thairu (the African Civilization) anawashangaa wale wote wanaodharau mavazi yetu na kukumbatia mavazi ya kigeni yasyojali hali ya hewa na mazingira ya nchi zetu za kiafrika. Mavazi haya ya kigeni tunayoyavaa sit u kwamba yanashindwa kututambulisha sisi ni kina nani bali yanatufanya tukose sababu ya kusheherekea uhuru wan chi yetu.

Kwa jinsi kila kitu kilivyokuwa kikifanyika pale mnazi mmoja huku kila mmoja akiwa katika vazi lake ni uthibitisho tosha kwamba kwa sasa tuko huru kweli kweli na mwingereza hana chake tena..

Jukwaa zima lilikuwa limetawaliwa na mavazi ambayo hayakuonesha maana ya kusheherekea uhuru wetu. Miaka 45 ya kujitawala ni mingi sana kuweza kujiamulia ni nini tunapenda kuvaa, baadhi yetutumechagua kuuvaa umagharibi ndani ya umaskini wa uhuru.
Natambua juhudi zilizofanywa na baadhi ya watu waliokuwa na mapenzi ya kutupatia watanzania kitambulisho kwa kubuni vazi la taifa. Hii ilikuwa nikipindi cha miaka ya 2000 na ninakumbuka kwamba baadhi ya wabunifu walifika mpaka kule Dodoma nyumbani kwa bunge la watanzania.


Kama ilivyo kawaida ya waswahili ‘watu wa ahadi’ suala hili sasa hakuna anayeliongelea na hata vazi lililoshinda nadhani sasa litakuwa limepambwa makumbusho kwa ajili ya kuvionesha vizazi vjavyo kwamba hili ni vazi la kitanzania ambalo halikuwavaliwa kwani wazazi wao walikuwa wakivaa mavazi mengine kwa kuwa tu walikuwa huru, wenye uwezo wa kujiamlia mabo yao wenyewe bila kuongozwa na mtu mwingine.

Kwangu mimi tofauti niliyoiona katika upande wa mavazi ina maanisha vitu vingi sana ikiwemo suala la kuibuka kwa matabaka katika jamii yetu. Matabaka ambayo yanashindwa kuelewa maana ya uhuru wa nchi yetu.

Mika hii 45 ya uhuru na mavazi yaliyovaliwa na wakati wa sherehe hizi na hasa yale ya viongozi wetu yanaonesha kabisa kuwa sasa uhuru wetu umekuwa ni kwa ajili ya kuchangisha pesa toka kwa wafanyabiashara wakubwa ili kufanikisha sherehe hizi ambapo mtanzania wa kawaida anaishia kukesha akiwa amevaa mavazi yasiyoeleka hasa mitumba huku viongozi wakijichana wakiwa ndani ya suti nzito zilizobuniwa na wabunifu toka kwa wale tuliokuwatukiwaita wakoloni na mabeberu.

Kwa kuona kwamba katika sherehe hizi hakuna aliyekuwa uchi, basi sula la vazi la taifa si muhimu hasa ukizingatia kuwa nchi yetu na utawala huu una mambo mengi ya kuonesha sasa tuko huru. Kila mmoja amevaa nguo anayoitaka na kumudu kununua kutokana na ruhusa ya kipato chake. Kwa kuwa na mambo mengi ya kuleta maisha bora kwa kila mtanzania suala la mavazi si la kujadili kwa sasa
SIKUKUU NJEMA WASOMAJI!!!


Ni kipindi kingine tena msomaji wa blog hii ambapo wakristo wote wanaungana na wenzao wengi duniani katika kusheherekea sherehe 'birthday' ya mkombozi wa maisha yao Bwana yesu Kristo. Hii ni siku kubwa na inatukumbusha juu ya nafasi yetu tuliyonayo katika kutekeleza lile lililotuleta duniani na tunahitajika tufanye nini ili tuingie mbinguni(kwa wanaoamini katika hili tu-wakristo)
Machweo inapenda kuwatakia watu wote msimu mzuri wa sikukuuza 2006 pamoja na Heri ya mwaka mpya 2007

Monday, December 18, 2006


CHUO KIKUU BILA MAKTABA!
Huu ni ukweli! Unashangaa chuo kimoja hapa mjini tena cha serikali kinatoa elimu ya juu bila kuwa na maktaba ambayo jengo lipo ila linakarabatiwa. Tunaunda wasomi wa vitini na madesa. Hii ndo bongo kila kitu usanii, fikiria mkandarasi wa kujenga jengo la wizara ya maendeleo ya jamii amemaliza jengo la ghorofa saba na kumshinda mkandarasi wa hapa chuoni ambaye alikuwa na kazi ya kukarabati milango na kupaka rangi, hii tenda ina walakini kwani wanaoumia ni wanaolipia huduma hii ya elimu na wanaofaidika na ukosefu wa maktaba ni wale waliosaini mkataba wa kuruhusu ukarabati.

Ukarabati umechukua miezi minne na sehemu na mpaka sasa hakuna kilichokabidhiwa kwa chuo ila jengo linang'aa kwa rangi nyeupe
LONGOLONGO ZA RICHMOND! KUNA 'WAKUBWA' HAPO

Mmeyasikia wenyewe, hakuna haja ya kuyarudia kuyaandika malumbano yanyoendelea kati ya shirika la ugavi la tanesco na 'wasanii' wanaojiita richmond. Hawa waliingia mkataba wa kuzalisha megawati 100 za umeme kwa kutumia majenereta yao waliyotoa marikani na kuiuzia tanesko. mitambo iliwasili na baada ya mbwembe nyingi sana za kuahidi kuzalisha kwanza megawati 20 kabla ya tarehe 1desemba2006 huku wakisaidiwa na waziri wa nishati, hakuna umeme uliozalishwa.
Sasa wamekuja na longolongo ya kusema kwamba eti tanesco imewapatia gesi chafu yenye kokoto! ukiniambia gesi kuwa na kokoto kwangu mimi nitakushangaa, hivi kumbe gesi ina kokoto kama zile za kujengea zege!
bado ninalia na wale wote waliofunga mkataba na kampuni hili linalodai lina makazi yake marekani huku mwakilishi wake hapa akiwa na mkoba tu, huu ni usanii

Hivi JK anasubiri nini kuwawajibisha wanasiasa waliosani mkataba huu, wakati mwingine ninajiuliza kama waziri mkuu alikuwa na sababu ya kulijibu shairi la bwana Marwa akijitapa kuwaonesha viongozi waadilifu waliojaa tele hapa nchini, yaani wamejaa tele halafu wafunge mikataba mibovu kama hii na bado waendelee kuwa wasafi na waliojaa tele.

Jeshi la polisi lipewe kazi ya kuwasaka wote 'waliojaa tele' na kusaini mkataba huu ili wafikishwe mahakamani na sheria ichukue mkondo wake! (unakumbuka enzi za kufilisiwa)

majambazi yakikamatwa basi tv zitarusha sana ama kibaka akiwa mikononi mwa wanachi wenye hasira, kila mmoja hunyanyua mkono ili amwadhibu kibaka lakini majambazi ya peni hapa kwetu yana heshimika sana na wanaonekana mahujaa, naamini kabisa richmond wamekula na 'waliojaa tele' na wanaendelea kutanua katika magari yenye viyoyozi kwani tarehe za pcb ni nyingi kurekebisha na kuua so.
Kaeni kimya mkisubiri uongo mwingine toka kwa wasanii wa Richmond

Monday, December 04, 2006

WASOMI WETU NA MIKATABA FEKI


Usiogope. Nadhani unakumbuka enzi za akina chifu Mangungo wa msovero na lile jasusi la kijerumani Karl Peters, enzi hizo watawala wetu walilazimishwa na kulazimika kusaini mikataba feki iliyowafanya wapoteze tawala zao katika nchi walizokuwa wanazitawala.

Kuna sababu nyingi zilizowanya wasaini mikataba hii, moja kubwa ikiwa ni ile hali ya kujua kusoma na kuandika lugha za kigeni. pamoja na kusaini mikataba hii feki watawala hawa wa kiafrika walikuwa wakichukua muda kuijadili na kuifikiri mikiataba hii.

Tofauti na sasa ambapo watu tuliowaamini katika kuongoza nchi yetu tajiri yenye watu wapole na wakarimu, ndio wanaotuumiza na kutufanya tukae gizani kwa kuingia mikataba ya kutunyanyasa huku wao wakifaidi 'aksante' waliyopewa na mambazi haya.

Fikiria mikataba yote ambayo serikali yetu imesaini, fikiria ile ya madini, IPTL na sasa huu mpya wa sijui inaitwa Richmond, hivi mikataba hii inamsaidia nini mtanzania wa kawaida. Ninasema wa kawaida kwa sababu sasa watanzania tunatofautiana, tuna matabaka yaani ni kama nchi za kibepali.

Mikataba hii walioisaini wapo, tunawajua na wanaendelea kula kuku tu na huku wakituimbia nyimbo za kutukaririsha ya kuwa uchumi wetu unakua! unakua au unakuwa!

Mimi si mchumi lakini siamini ukuaji wa uchumi huku nchi ikiwa haina umeme wa uhakika, ni mgao tu kwa kwenda mbele huku wale tuliowaamini kutuwakilisha bungeni wanakaa kimya na kujadili mambo hata yenye jibu tayari, wanajadili eti kuhusu vazi la spika, inamaana spika yuko uchi au wanadhani wakimnunulia spika vazi jipya ndipo watajadili hoja tunazotaka wazijadiliili.

Kwanza hilojoho akilifua atalinyoosha na nini? OOOps nilisahau kumbe wao ni tofauti na mimi, wao kila siku ni full kipupwe, full kiyoyozii
WASOMI WETU NA MIKATABA FEKI


Usiogope. Nadhani unakumbuka enzi za akina chifu Mangungo wa msovero na lile jasusi la kijerumani Karl Peters, enzi hizo watawala wetu walilazimishwa na kulazimika kusaini mikataba feki iliyowafanya wapoteze tawala zao katika nchi walizokuwa wanazitawala.

Kuna sababu nyingi zilizowanya wasaini mikataba hii, moja kubwa ikiwa ni ile hali ya kujua kusoma na kuandika lugha za kigeni. pamoja na kusaini mikataba hii feki watawala hawa wa kiafrika walikuwa wakichukua muda kuijadili na kuifikiri mikiataba hii.

Tofauti na sasa ambapo watu tuliowaamini katika kuongoza nchi yetu tajiri yenye watu wapole na wakarimu, ndio wanaotuumiza na kutufanya tukae gizani kwa kuingia mikataba ya kutunyanyasa huku wao wakifaidi 'aksante' waliyopewa na mambazi haya.

Fikiria mikataba yote ambayo serikali yetu imesaini, fikiria ile ya madini, IPTL na sasa huu mpya wa sijui inaitwa Richmond, hivi mikataba hii inamsaidia nini mtanzania wa kawaida. Ninasema wa kawaida kwa sababu sasa watanzania tunatofautiana, tuna matabaka yaani ni kama nchi za kibepali.

Mikataba hii walioisaini wapo, tunawajua na wanaendelea kula kuku tu na huku wakituimbia nyimbo za kutukaririsha ya kuwa uchumi wetu unakua! unakua au unakuwa!

Mimi si mchumi lakini siamini ukuaji wa uchumi huku nchi ikiwa haina umeme wa uhakika, ni mgao tu kwa kwenda mbele huku wale tuliowaamini kutuwakilisha bungeni wanakaa kimya na kujadili mambo hata yenye jibu tayari, wanajadili eti kuhusu vazi la spika, inamaana spika yuko uchi au wanadhani wakimnunulia spika vazi jipya ndipo watajadili hoja tunazotaka wazijadiliili.

Kwanza hilojoho akilifua atalinyoosha na nini? OOOps nilisahau kumbe wao ni tofauti na mimi, wao kila siku ni full kipupwe, full kiyoyozii